Isaya 42:1-25 ONEN
[1] “Huyu hapa mtumishi wangu, ninayemtegemeza, mteule wangu, ambaye ninapendezwa naye; nitaweka Roho yangu juu yake, naye ataleta haki kwa mataifa. [2] Hatapaza sauti wala kupiga kelele, wala hataiinua sauti yake barabarani. [3] Mwanzi uliopondeka hatauvunja, na utambi unaofuka moshi hatauzima. Kwa uaminifu ataleta haki, [4] hatazimia roho wala kukata tamaa, mpaka atakaposimamisha haki juu ya dunia. Visiwa vitaweka tumaini lao katika sheria yake.” [5] Hili ndilo asemalo Mungu, BWANA, yeye aliyeziumba mbingu na kuzitanda, aliyeitandaza dunia na vyote vitokavyo humo, awapaye watu wake pumzi, na uzima kwa wale waendao humo: [6] “Mimi, BWANA, nimekuita katika haki; nitakushika mkono wako. Nitakulinda na kukufanya kuwa Agano kwa ajili ya watu na nuru kwa Mataifa, [7] kuwafungua macho wale wasioona, kuwaacha huru kutoka kifungoni waliofungwa jela, na kuwafungua kutoka gerezani wale wanaokaa gizani. [8] “Mimi ndimi BWANA; hilo ndilo Jina langu! Sitampa mwingine utukufu wangu wala sanamu sifa zangu. [9] Tazama, mambo ya kwanza yametokea, nami natangaza mambo mapya; kabla hayajatokea nawatangazia habari zake.” [10] Mwimbieni BWANA wimbo mpya, sifa zake toka miisho ya dunia, ninyi mshukao chini baharini, na vyote vilivyomo ndani yake, enyi visiwa na wote wakaao ndani yake. [11] Jangwa na miji yake na vipaze sauti zao; makao anamoishi Kedari na yashangilie. Watu wa Sela waimbe kwa furaha, na wapige kelele kutoka vilele vya milima. [12] Wampe BWANA utukufu, na kutangaza sifa zake katika visiwa. [13] BWANA ataenda kama mtu mwenye nguvu, kama shujaa atachochea shauku yake, kwa kelele ataamsha kilio cha vita, naye atashinda adui zake. [14] “Kwa muda mrefu nimenyamaza kimya, nimekaa kimya na kujizuia. Lakini sasa, kama mwanamke wakati wa kujifungua, ninapiga kelele, ninatweta na kushusha pumzi. [15] Nitaharibu milima na vilima na kukausha mimea yako yote; nitafanya mito kuwa visiwa na kukausha mabwawa. [16] Nitawaongoza vipofu kwenye njia ambayo hawajaijua, kwenye mapito wasiyoyazoea nitawaongoza; nitafanya giza kuwa nuru mbele yao, na kufanya mahali palipoparuza kuwa laini. Haya ndiyo mambo nitakayofanya; mimi sitawaacha. [17] Lakini wale wanaotumaini sanamu, wanaoviambia vinyago, ‘Ninyi ndio miungu yetu,’ watarudishwa nyuma kwa aibu kubwa. [18] “Sikieni, enyi viziwi; tazameni, enyi vipofu, mpate kuona! [19] Ni nani aliye kipofu isipokuwa mtumishi wangu, na kiziwi kama mjumbe ninayemtuma? Ni nani aliye kipofu kama yeye aliyejitoa kwangu, aliye kipofu kama mtumishi wa BWANA? [20] Mmeona vitu vingi, lakini hamkuzingatia; masikio yenu yako wazi, lakini hamsikii chochote.” [21] Ilimpendeza BWANA kwa ajili ya haki yake kufanya sheria yake kuwa kuu na tukufu. [22] Lakini hili ni taifa lililoibwa na kutekwa nyara, wote wamenaswa katika mashimo, au wamefichwa katika magereza. Wamekuwa nyara, wala hapana yeyote awaokoaye. Wamefanywa mateka, wala hapana yeyote asemaye, “Warudishe.” [23] Ni nani miongoni mwenu atakayesikiliza hili, au atakayezingatia kwa makini katika wakati ujao? [24] Ni nani aliyemtoa Yakobo kuwa mateka, na Israeli kwa wateka nyara? Je, hakuwa yeye, BWANA, ambaye tumetenda dhambi dhidi yake? Kwa kuwa hawakufuata njia zake, hawakutii sheria zake. [25] Hivyo akawamwagia hasira yake inayowaka, ukali wa vita. Iliwazunguka kwa miali ya moto, lakini hata hivyo hawakuelewa; iliwateketeza, lakini hawakuyatia moyoni.
