Isaya 38:1-22 ONEN
[1] Katika siku hizo Hezekia akaugua, naye akawa karibu kufa. Nabii Isaya mwana wa Amozi akaenda kwake na kumwambia, “Hili ndilo asemalo BWANA: Tengeneza mambo ya nyumba yako, kwa sababu utakufa, hutapona.” [2] Hezekia akaelekeza uso wake ukutani, akamwomba BWANA: [3] “Ee BWANA, kumbuka jinsi nilivyoenenda mbele zako kwa uaminifu na kujitoa kwa moyo wangu wote, na kufanya yaliyo mema machoni pako.” Naye Hezekia akalia kwa uchungu. [4] Ndipo neno la BWANA likamjia Isaya, kusema: [5] “Nenda ukamwambie Hezekia, ‘Hili ndilo asemalo BWANA, Mungu wa baba yako Daudi: Nimeyasikia maombi yako na nimeona machozi yako. Nitakuongezea miaka kumi na mitano katika maisha yako. [6] Nami nitakuokoa wewe pamoja na mji huu mkononi mwa mfalme wa Ashuru. Nitaulinda mji huu. [7] “ ‘Hii ndiyo ishara ya BWANA kwako ya kwamba BWANA atafanya kile alichoahidi: [8] Nitafanya kivuli cha jua kwenye ngazi iliyojengwa na Ahazi kirudi nyuma madaraja kumi.’ ” Hivyo jua likarudi nyuma madaraja kumi ambayo lilikuwa limeshuka. [9] Maandiko ya Hezekia mfalme wa Yuda baada ya kuugua kwake na kupona: [10] Nilisema, “Katika ustawi wa maisha yangu, je, ni lazima nipite katika malango ya mauti, na kupokonywa miaka yangu iliyobaki?” [11] Nilisema, “Sitamwona tena BWANA, BWANA katika nchi ya walio hai, wala sitamtazama tena mwanadamu, wala kuwa na wale ambao sasa wanakaa katika ulimwengu huu. [12] Kama hema la mchunga mifugo, nyumba yangu imebomolewa na kutwaliwa kutoka kwangu. Kama mfumaji nimevingirisha maisha yangu, naye amenikatilia mbali kutoka kitanda cha mfumi. Mchana na usiku uliyakomesha maisha yangu. [13] Nilingoja kwa uvumilivu hadi mapambazuko, lakini alivunja mifupa yangu yote kama simba. Mchana na usiku uliyakomesha maisha yangu. [14] Nililia kama mbayuwayu au korongo, niliomboleza kama hua aombolezaye. Macho yangu yalififia nilipotazama mbinguni. Ee Bwana, ninataabika, njoo unisaidie!” [15] Lakini niseme nini? Amesema nami, naye yeye mwenyewe amelitenda hili. Nitatembea kwa unyenyekevu katika miaka yangu yote kwa sababu ya haya maumivu makali ya nafsi yangu. [16] Bwana, kwa mambo kama haya watu huishi, nayo roho yangu hupata uzima katika hayo pia. Uliniponya na kuniacha niishi. [17] Hakika ilikuwa ya faida yangu ndiyo maana nikapata maumivu makali. Katika upendo wako ukaniokoa kutoka shimo la uharibifu; umeziweka dhambi zangu zote nyuma yako. [18] Kwa maana kaburi haliwezi kukusifu, mauti haiwezi kuimba sifa zako; wale washukao chini shimoni hawawezi kuutarajia uaminifu wako. [19] Walio hai, walio hai: hao wanakusifu, kama ninavyofanya leo. Baba huwaambia watoto wao habari za uaminifu wako. [20] BWANA ataniokoa, nasi tutaimba kwa vyombo vya nyuzi siku zote za maisha yetu katika Hekalu la BWANA. [21] Isaya alikuwa amesema, “Tengenezeni dawa ya kubandika ya tini, mweke juu ya jipu, naye atapona.” [22] Hezekia alikuwa ameuliza, “Kutakuwa na ishara gani kwamba nitapanda kwenda Hekalu la BWANA?”
