Isaya 32:1-20 ONEN
[1] Tazama, mfalme atatawala kwa uadilifu na watawala watatawala kwa haki. [2] Kila mtu atakuwa kama kivuli cha kujificha kutokana na upepo na kimbilio kutokana na dhoruba, kama vijito vya maji jangwani na kivuli cha mwamba mkubwa katika ardhi yenye kiu. [3] Ndipo macho ya wale wanaoona hayatafumbwa tena, nayo masikio ya wale wanaosikia yatasikiliza. [4] Moyo wa mtu mwenye hamaki utafahamu na kuelewa, nao ulimi wenye kigugumizi utanena kwa ufasaha. [5] Mpumbavu hataitwa tena muungwana, wala mtu mbaya kabisa kupewa heshima ya juu. [6] Kwa kuwa mpumbavu hunena upumbavu, moyo wake hushughulika na uovu: Hutenda mambo yasiyo ya kumcha Mungu, na hueneza habari za makosa kuhusu BWANA; yeye huwaacha wenye njaa bila kitu, na wenye kiu huwanyima maji. [7] Taratibu za mtu mbaya kabisa ni ovu, hufanya mipango miovu ili kumwangamiza maskini kwa uongo, hata wakati ambapo hoja za mhitaji ni za haki. [8] Lakini mtu muungwana hufanya mipango ya kiungwana, na kwa matendo ya kiungwana yeye hufanikiwa. [9] Enyi wanawake wenye kuridhika sana, amkeni na mnisikilize. Enyi binti mnaojisikia kuwa salama, sikieni lile ninalotaka kuwaambia! [10] Muda zaidi kidogo ya mwaka mmoja, ninyi mnaojisikia salama mtatetemeka, mavuno ya zabibu yatakoma na mavuno ya matunda hayatakuwepo. [11] Tetemekeni, enyi wanawake wenye kuridhika, tetemekeni kwa hofu, enyi binti mnaojisikia salama! Vueni nguo zenu, vaeni nguo ya gunia viunoni mwenu. [12] Pigeni matiti yenu kwa ajili ya mashamba mazuri, kwa ajili ya mizabibu iliyozaa vizuri [13] na kwa ajili ya nchi ya watu wangu, nchi ambayo miiba na michongoma imemea: naam, ombolezeni kwa ajili ya nyumba zote za furaha na kwa ajili ya mji huu wenye kufanya sherehe. [14] Ngome itaachwa, mji wenye kelele nyingi utahamwa, ngome ndani ya mji na mnara wa ulinzi vitakuwa ukiwa milele, mahali pazuri pa punda na malisho ya makundi ya kondoo, [15] mpaka Roho amwagwe juu yetu kutoka juu, nalo jangwa kuwa shamba lenye rutuba, na shamba lenye rutuba kuwa kama msitu. [16] Haki itakaa katika jangwa, na uadilifu utakaa katika shamba lenye rutuba. [17] Matunda ya haki yatakuwa amani, matokeo ya haki yatakuwa utulivu na matumaini milele. [18] Watu wangu wataishi katika makao ya mahali pa amani, katika nyumba zilizo salama, katika mahali pa kupumzika pasipo na usumbufu. [19] Hata kama mvua ya mawe iangushe msitu na mji ubomolewe kabisa, [20] tazama jinsi utakavyobarikiwa, ukipanda mbegu yako katika kila kijito, na kuwaacha ngʼombe wako na punda wajilishe kwa uhuru.
