Isaya 3:1-26 ONEN
[1] Tazama sasa, Bwana, BWANA Mwenye Nguvu Zote, yu karibu kuwaondolea Yerusalemu na Yuda upatikanaji wa mahitaji na misaada, upatikanaji wote wa chakula na tegemeo lote la maji, [2] shujaa na mtu wa vita, mwamuzi na nabii, mwaguzi na mzee, [3] jemadari wa kikosi cha watu hamsini na mtu mwenye cheo, mshauri, fundi stadi na mlozi mjanja. [4] Nitawafanya wavulana wawe maafisa wao, watoto ndio watakaowatawala. [5] Watu wataoneana wao kwa wao: mtu dhidi ya mtu, na jirani dhidi ya jirani yake. Kijana atainuka dhidi ya mzee, mtu mnyonge dhidi ya mtu mwenye heshima. [6] Mtu atamkamata mmoja wa ndugu zake katika nyumba ya baba yake na kusema, “Unalo joho, sasa uwe kiongozi wetu, tawala lundo hili la magofu!” [7] Lakini siku hiyo atapiga kelele akisema, “Sina uponyaji. Sina chakula wala mavazi katika nyumba yangu, msinifanye niwe kiongozi wa watu.” [8] Yerusalemu inapepesuka, Yuda inaanguka; maneno yao na matendo yao ni kinyume na BWANA, wakiudharau uwepo wake uliotukuka. [9] Nyuso zao zinavyoonekana zinashuhudia dhidi yao, hujivunia dhambi yao kama Sodoma, wala hawaifichi. Ole wao! Wamejiletea maafa juu yao wenyewe. [10] Waambie wanyofu itakuwa heri kwao, kwa kuwa watafurahia tunda la matendo yao. [11] Ole kwa watu waovu! Maafa yapo juu yao! Watalipwa kwa ajili ya yale mikono yao iliyotenda. [12] Vijana wanawatesa watu wangu, wanawake wanawatawala. Enyi watu wangu, viongozi wenu wanawapotosha, wanawapoteza njia. [13] BWANA anachukua nafasi yake mahakamani, anasimama kuhukumu watu. [14] BWANA anaingia katika hukumu dhidi ya wazee na viongozi wa watu wake: “Ninyi ndio mlioharibu shamba langu la mizabibu, mali zilizonyangʼanywa maskini zimo nyumbani mwenu. [15] Mnamaanisha nini kuwaponda watu wangu na kuzisaga nyuso za maskini?” asema Bwana, BWANA Mwenye Nguvu Zote. [16] BWANA asema, “Wanawake wa Sayuni wana kiburi, wanatembea na shingo ndefu, wakikonyeza kwa macho yao, wanatembea kwa hatua za madaha, wakiwa na mapambo ya njuga kwenye vifundo vya miguu yao. [17] Kwa hiyo Bwana ataleta majipu kwenye vichwa vya wanawake wa Sayuni; BWANA atazifanya ngozi za vichwa vyao kuwa vipara.” [18] Katika siku ile Bwana atawanyangʼanya uzuri wao: bangili, tepe za kichwani, mikufu yenye alama za mwezi mwandamo, [19] vipuli, vikuku, shela, [20] vilemba, mikufu ya vifundo vya miguu, mshipi, chupa za manukato na hirizi, [21] pete zenye muhuri, pete za puani, [22] majoho mazuri, mitandio, mavazi, kifuko cha kutilia fedha, [23] vioo, mavazi ya kitani, taji na shali. [24] Badala ya harufu ya manukato kutakuwa na uvundo; badala ya mishipi, ni kamba; badala ya nywele zilizotengenezwa vizuri, ni upara; badala ya mavazi mazuri, ni nguo za magunia; badala ya uzuri, ni alama ya aibu kwa chuma cha moto. [25] Wanaume wako watauawa kwa upanga, nao mashujaa wako watauawa vitani. [26] Malango ya Sayuni yataomboleza na kulia, ataketi mavumbini akiwa fukara.
