[1] Neno kuhusu Jangwa kando ya Bahari: Kama upepo wa kisulisuli unaopita katika nchi hadi kusini, mshambuliaji anakuja kutoka jangwani, kutoka nchi inayotisha. [2] Nimeonyeshwa maono ya kutisha: Msaliti anasaliti, mteka nyara anateka nyara. Elamu, shambulia! Umedi, izunguke kwa jeshi! Nitakomesha huzuni zote alizosababisha. [3] Katika hili mwili wangu umeteswa na maumivu, maumivu makali ya ghafula yamenishika, kama yale ya mwanamke mwenye utungu wa kuzaa. Nimeduwazwa na lile ninalolisikia, nimeshangazwa na lile ninaloliona. [4] Moyo wangu unababaika, woga unanifanya nitetemeke, gizagiza la jioni nililolitamani sana, limekuwa hofu kuu kwangu. [5] Wanaandaa meza, wanatandaza mazulia, wanakula, wanakunywa! Amkeni, enyi maafisa, zitieni ngao mafuta! [6] Hili ndilo Bwana analoniambia: “Nenda, weka mlinzi, na atoe taarifa ya kile anachokiona. [7] Anapoona magari ya vita pamoja na kundi la farasi, wapanda punda au wapanda ngamia, na awe macho, awe macho kikamilifu.” [8] Naye mlinzi alipaza sauti, “Mchana baada ya mchana, bwana wangu, ninasimama katika mnara wa ulinzi, kila usiku ninakaa mahali pangu nilipoamriwa. [9] Tazama, yuaja mtu anayepanda gari la vita pamoja na kundi la farasi. Naye anajibu: ‘Babeli umeanguka, umeanguka! Vinyago vyote vya miungu yake vimelala chini vikiwa vimevunjwa!’ ” [10] Ee watu wangu, mliopondwa kwenye sakafu ya kupuria, ninawaambia kile nilichokisikia kutoka kwa BWANA Mwenye Nguvu Zote, kutoka kwa Mungu wa Israeli. [11] Neno kuhusu Duma: Mtu fulani ananiita kutoka Seiri, “Mlinzi, usiku utaisha lini? Mlinzi, usiku utaisha lini?” [12] Mlinzi anajibu, “Asubuhi inakuja, lakini pia usiku. Kama ungeliuliza, basi uliza; bado na urudi tena.” [13] Neno kuhusu Arabia: Enyi misafara ya Wadedani, mnaopiga kambi katika vichaka vya Arabia, [14] leteni maji kwa wenye kiu, ninyi mnaoishi Tema, leteni chakula kwa ajili ya wakimbizi. [15] Wanaukimbia upanga, kutoka upanga uliochomolewa alani, kutoka upinde uliopindwa, na kutoka kwenye joto la vita. [16] Hili ndilo Bwana analoniambia: “Katika muda wa mwaka mmoja, kama vile mtumishi aliyefungwa na mkataba angeihesabu, majivuno yote ya Kedari yatafikia mwisho. [17] Wanaume wavutao pinde walionusurika, mashujaa wa Kedari, watakuwa wachache.” BWANA, Mungu wa Israeli, amesema.