Isaya 19:1-25 ONEN
[1] Neno kuhusu Misri: Tazama, BWANA amepanda juu ya wingu liendalo kwa haraka naye anakuja Misri. Sanamu za Misri zinatetemeka mbele yake, nayo mioyo ya Wamisri inayeyuka ndani yao. [2] “Nitamchochea Mmisri dhidi ya Mmisri, ndugu atapigana dhidi ya ndugu, jirani dhidi ya jirani, mji dhidi ya mji, ufalme dhidi ya ufalme. [3] Wamisri watakufa moyo, na nitaibatilisha mipango yao. Watatafuta ushauri kwa sanamu na kwa roho za waliokufa, kwa waaguzi na kwa wale waongeao na mizimu. [4] Nitawatia Wamisri mikononi mwa bwana mkatili na mfalme mkali atatawala juu yao,” asema Bwana, BWANA Mwenye Nguvu Zote. [5] Maji ya mito yatakauka, chini ya mto kutakauka kwa jua. [6] Mifereji itanuka; vijito vya Misri vitapungua na kukauka. Mafunjo na nyasi vitanyauka, [7] pia mimea iliyoko kando ya Mto Naili, pale mto unapomwaga maji baharini. Kila shamba lililopandwa kando ya Mto Naili litakauka, litapeperushwa na kutoweka kabisa. [8] Wavuvi watalia na kuomboleza, wale wote watupao ndoano katika Mto Naili, watadhoofika kwa majonzi. [9] Wale watu wafanyao kazi ya kitani kilichochambuliwa watakata tamaa, wafumaji wa kitani safi watavunjika moyo. [10] Wafanyao kazi ya kufuma nguo watahuzunishwa, nao vibarua wataugua moyoni. [11] Maafisa wa Soani ni wapumbavu kabisa, washauri wa Farao wenye busara wanatoa ushauri wa kijinga. Unawezaje kumwambia Farao, “Mimi ni mmojawapo wa watu wenye hekima, mwanafunzi wa wafalme wa zamani”? [12] Wako wapi sasa watu wako wenye hekima? Wao wakuonyeshe na kukufahamisha ni nini BWANA Mwenye Nguvu Zote amepanga dhidi ya Misri. [13] Maafisa wa Soani wamekuwa wapumbavu, viongozi wa Memfisi wamedanganyika, walio mawe ya pembe ya taifa lake wameipotosha Misri. [14] BWANA amewamwagia roho ya kizunguzungu; wanaifanya Misri iyumbayumbe katika yale yote inayoyafanya, kama vile mlevi ayumbayumbavyo katika kutapika kwake. [15] Misri haiwezi kufanya kitu chochote, cha kichwa wala cha mkia, cha tawi la mtende wala cha tete. [16] Katika siku ile Wamisri watakuwa kama wanawake. Watatetemeka kwa hofu mbele ya mkono wa BWANA Mwenye Nguvu Zote anaoinua dhidi yao. [17] Nayo nchi ya Yuda itawatia hofu Wamisri, kila mmoja atakayetajiwa Yuda ataingiwa na hofu, kwa sababu ya kile ambacho BWANA Mwenye Nguvu Zote anapanga dhidi yao. [18] Katika siku hiyo miji mitano ya Misri, itazungumza lugha ya Kanaani, na kuapa kumtii BWANA Mwenye Nguvu Zote. Mji mmojawapo utaitwa Mji wa Uharibifu. [19] Katika siku hiyo patakuwepo madhabahu ya BWANA katikati ya Misri na mnara wa kumbukumbu kwa BWANA kwenye mpaka wa Misri. [20] Itakuwa alama na ushahidi kwa ajili ya BWANA Mwenye Nguvu Zote katika nchi ya Misri. Watakapomlilia BWANA kwa sababu ya watesi wao, Mungu atawapelekea mwokozi na mtetezi, naye atawaokoa. [21] Hivyo BWANA atajijulisha mwenyewe kwa Wamisri, nao katika siku hiyo watamkubali BWANA. Wataabudu kwa kumtolea dhabihu na sadaka za nafaka, watamwekea BWANA nadhiri na kuzitimiza. [22] BWANA ataipiga Misri kwa tauni; atawapiga na kuwaponya. Watamgeukia BWANA, naye atayasikia maombi yao na kuwaponya. [23] Katika siku hiyo kutakuwepo na njia kuu kutoka Misri hadi Ashuru. Waashuru watakwenda Misri, na Wamisri watakwenda Ashuru. Wamisri na Waashuru wataabudu pamoja. [24] Katika siku hiyo Israeli itakuwa ya tatu, pamoja na Misri na Ashuru, nao watakuwa baraka kwa dunia. [25] BWANA Mwenye Nguvu Zote atawabariki, akisema, “Baraka iwe kwa Misri watu wangu, kwa Ashuru kazi ya mikono yangu, na kwa Israeli urithi wangu.”
