[1] “Wakati Israeli alipokuwa mtoto, nilimpenda, nilimwita mwanangu kutoka Misri. [2] Lakini kadiri nilivyomwita Israeli, ndivyo walivyokwenda mbali nami. Walitoa dhabihu kwa Mabaali na kufukiza uvumba kwa vinyago. [3] Mimi ndiye niliyemfundisha Efraimu kutembea, nikiwashika mikono; lakini hawakutambua kuwa ni mimi niliyewaponya. [4] Niliwaongoza kwa kamba za huruma ya kibinadamu, kwa vifungo vya upendo; niliondoa nira shingoni mwao nami nikainama kuwalisha. [5] “Je, hawatarudi Misri, nayo Ashuru haitawatawala kwa sababu wamekataa kutubu? [6] Panga zitametameta katika miji yao, zitaharibu makomeo ya malango yao na kukomesha mipango yao. [7] Watu wangu wamedhamiria kuniacha. Hata kama wakimwita Yeye Aliye Juu Sana, kwa vyovyote hatawainua. [8] “Efraimu, ninawezaje kukuacha? Ee Israeli, ninawezaje kukutoa? Nitawezaje kukutendea kama Adma? Nitawezaje kukufanya kama Seboimu? Moyo wangu umegeuka ndani yangu, huruma zangu zote zimeamshwa. [9] Sitatimiza hasira yangu kali, wala sitageuka na kumharibu Efraimu. Kwa kuwa mimi ndimi Mungu, wala si mwanadamu, Aliye Mtakatifu miongoni mwenu. Sitakuja kwa ghadhabu. [10] Watamfuata BWANA; atanguruma kama simba. Wakati angurumapo, watoto wake watakuja wakitetemeka kutoka magharibi. [11] Watakuja wakitetemeka kama ndege wakitoka Misri, kama hua wakitoka Ashuru. Nitawakalisha katika nyumba zao,” asema BWANA. [12] Efraimu amenizunguka kwa uongo, nyumba ya Israeli kwa udanganyifu. Naye Yuda ni mkaidi dhidi ya Mungu, hata kinyume cha yule mwaminifu Aliye Mtakatifu.