Hesabu 34:1-29 ONEN
[1] BWANA akamwambia Mose, [2] “Waamuru Waisraeli na uwaambie: ‘Mtakapoingia nchi ya Kanaani, nchi ambayo itagawanywa kwenu kama urithi itakuwa na mipaka ifuatayo: [3] “ ‘Upande wenu wa kusini utajumuisha sehemu ya Jangwa la Sini kufuata mpaka wa Edomu. Upande wa mashariki mpaka wenu wa kusini utaanzia mwisho wa Bahari ya Chumvi, [4] katiza kusini mwa Pito la Akrabimu, endelea mpaka Sini na kwenda kusini ya Kadesh-Barnea. Kisha mpaka huo utaenda hadi Hasar-Adari hadi Azmoni, [5] mahali ambapo utapinda, na kuunganika na Kijito cha Misri na kumalizikia kwenye Bahari ya Kati. [6] “ ‘Mpaka wenu wa magharibi utakuwa Bahari ya Kati. Huu utakuwa mpaka wenu upande wa magharibi. [7] “ ‘Kwa mpaka wenu wa kaskazini, wekeni alama kuanzia Bahari ya Kati hadi mlima Hori, [8] na kutoka mlima Hori hadi Pito la Hamathi. Kisha mpaka utaenda hadi Sedadi, [9] kuendelea hadi Zifroni, na kuishia Hasar-Enani. Huu utakuwa mpaka wenu upande wa kaskazini. [10] “ ‘Kwa mpaka wenu wa mashariki, wekeni alama kuanzia Hasar-Enani hadi Shefamu. [11] Mpaka utaelekea kusini kuanzia Shefamu hadi Ribla upande wa mashariki wa Aini, na kuendelea kwenye miteremko mashariki mwa Bahari ya Kinerethi. [12] Kisha mpaka utashuka kuelekea Mto Yordani na kuishia katika Bahari ya Chumvi. “ ‘Hii itakuwa nchi yenu, ikiwa na mipaka yake kila upande.’ ” [13] Mose akawaamuru Waisraeli: “Gawanyeni nchi hii kwa kura kama urithi. BWANA ameagiza kwamba itolewe kwa yale makabila tisa na nusu, [14] kwa sababu jamaa ya kabila la Reubeni, kabila la Gadi, na nusu ya kabila la Manase wamekwishapokea urithi wao. [15] Haya makabila mawili na nusu wamekwishapokea urithi wao upande wa mashariki wa Yordani ngʼambo ya Yeriko, kuelekea mawio ya jua.” [16] BWANA akamwambia Mose, [17] “Haya ndiyo majina ya watu ambao watakusaidia kugawanya nchi kama urithi: Eleazari kuhani na Yoshua mwana wa Nuni. [18] Tena uteue kiongozi mmoja kutoka kila kabila kusaidia kuigawanya nchi. [19] Haya ndiyo majina yao: “Kalebu mwana wa Yefune, kutoka kabila la Yuda; [20] Shemueli mwana wa Amihudi, kutoka kabila la Simeoni; [21] Elidadi mwana wa Kisloni, kutoka kabila la Benyamini; [22] Buki mwana wa Yogli, kiongozi kutoka kabila la Dani; [23] Hanieli mwana wa Efodi, kiongozi kutoka kabila la Manase mwana wa Yosefu; [24] Kemueli mwana wa Shiftani, kiongozi kutoka kabila la Efraimu mwana wa Yosefu; [25] Elisafani mwana wa Parnaki, kiongozi kutoka kabila la Zabuloni; [26] Paltieli mwana wa Azani, kiongozi kutoka kabila la Isakari; [27] Ahihudi mwana wa Shelomi, kiongozi kutoka kabila la Asheri; [28] Pedaheli mwana wa Amihudi, kiongozi kutoka kabila la Naftali.” [29] Hawa ndio watu ambao BWANA aliamuru wagawanye urithi kwa Waisraeli katika nchi ya Kanaani.
