Filemoni 1:1-25 ONEN
[1] Paulo, mfungwa wa Kristo Yesu, pamoja na Timotheo ndugu yetu: Kwa Filemoni rafiki yetu mpendwa na mtendakazi mwenzetu, [2] kwa dada yetu mpendwa Afia, kwa Arkipo askari mwenzetu na kwa kanisa lile likutanalo nyumbani mwako: [3] Neema iwe nanyi na amani itokayo kwa Mungu Baba yetu na Bwana Yesu Kristo. [4] Siku zote ninamshukuru Mungu ninapokukumbuka katika maombi yangu, [5] kwa sababu ninasikia juu ya imani yako katika Bwana Yesu na upendo wako kwa watakatifu wote. [6] Naomba utiwe nguvu katika kuishuhudia imani yako, ili upate kuwa na ufahamu mkamilifu juu ya kila kitu chema tulicho nacho ndani ya Kristo. [7] Upendo wako umenifurahisha mno na kunitia moyo, kwa sababu wewe ndugu, umeiburudisha mioyo ya watakatifu. [8] Hata hivyo, ingawa katika Kristo ningeweza kuwa na ujasiri na kukuagiza yale yakupasayo kutenda, [9] lakini ninakuomba kwa upendo, mimi Paulo, mzee na pia sasa nikiwa mfungwa wa Kristo Yesu, [10] nakuomba kwa ajili ya mwanangu Onesimo, aliyefanyika mwanangu nilipokuwa kwenye minyororo. [11] Mwanzoni alikuwa hakufai, lakini sasa anakufaa sana wewe na mimi pia. [12] Namtuma kwako, yeye aliye moyo wangu hasa. [13] Ningependa nikae naye ili ashike nafasi yako ya kunisaidia wakati huu nikiwa kifungoni kwa ajili ya Injili. [14] Lakini sikutaka kufanya lolote bila idhini yako, ili wema wowote uufanyao usiwe wa lazima, bali wa hiari. [15] Huenda sababu ya yeye kutengwa nawe kwa kitambo kidogo ni ili uwe naye daima. [16] Si kama mtumwa, bali bora kuliko mtumwa, kama ndugu mpendwa. Yeye ni mpendwa sana kwangu na hata kwako zaidi, yeye kama mwanadamu na kama ndugu katika Bwana. [17] Hivyo kama unanihesabu mimi kuwa mshirika wako, mkaribishe kama vile ungenikaribisha mimi mwenyewe. [18] Kama amekukosea lolote au kama unamdai chochote, nidai mimi. [19] Ni mimi Paulo, ninayeandika waraka huu kwa mkono wangu mwenyewe. Nitakulipa. Sitaji kwamba nakudai hata nafsi yako. [20] Ndugu yangu, natamani nipate faida kwako katika Bwana, uuburudishe moyo wangu katika Kristo. [21] Nikiwa na hakika ya utii wako, nakuandikia, nikijua kwamba utafanya hata zaidi ya yale ninayokuomba. [22] Jambo moja zaidi: Niandalie chumba cha wageni, kwa kuwa nataraji kurudishwa kwenu kama jibu la maombi yenu. [23] Epafra, aliye mfungwa mwenzangu katika Kristo Yesu, anakusalimu. [24] Vivyo hivyo Marko, Aristarko, Dema na Luka, watendakazi wenzangu wanakusalimu. [25] Neema ya Bwana Yesu Kristo iwe pamoja na roho zenu. Amen.
