Ezekieli 35:1-15 ONEN

[1] Neno la BWANA likanijia kusema: [2] “Mwanadamu, elekeza uso wako juu ya mlima Seiri, utabiri dhidi yake [3] na useme: ‘Hili ndilo BWANA Mwenyezi asemalo: Mimi ni kinyume nawe, ee mlima Seiri, nami nitanyoosha mkono wangu dhidi yako na kukufanya ukiwa na usiyekaliwa na watu wala kulimika. [4] Nitaifanya miji yako kuwa magofu nawe utakuwa ukiwa. Ndipo utakapojua kuwa Mimi ndimi BWANA. [5] “ ‘Kwa sababu ulificha moyoni uadui wa siku nyingi nawe ukawatoa Waisraeli wauawe kwa upanga wakati wa maafa yao, wakati adhabu yake ilipofikia kilele chake, [6] kwa hiyo hakika kama niishivyo, asema BWANA Mwenyezi, nitakutia katika umwagaji damu nao utakufuatia. Kwa kuwa hakuchukia kumwaga damu, kumwaga damu kutakufuatia. [7] Nitaufanya Mlima Seiri ukiwa na usiokaliwa na watu wala kulimika na kuukatilia mbali na wote wanaokuja na wanaokwenda. [8] Nitaijaza milima yenu kwa watu wake waliouawa, wale waliouawa kwa upanga wataanguka juu ya vilima vyako na katika mabonde yako na katika makorongo yako yote. [9] Nitakufanya ukiwa milele, watu hawataishi katika miji yako. Ndipo utakapojua kuwa Mimi ndimi BWANA. [10] “ ‘Kwa sababu umesema, “Mataifa haya mawili na nchi hizi zitakuwa zetu nasi tutazimiliki,” ingawa hata mimi BWANA nilikuwa huko, [11] kwa hiyo hakika kama niishivyo, asema BWANA Mwenyezi, nitakutenda kwa kadiri ya hasira na wivu uliouonyesha katika chuki yako juu yao nami nitafanya nijulikane miongoni mwao wakati nitakapokuhukumu. [12] Ndipo utakapojua kuwa Mimi BWANA nimesikia mambo yote ya dharau uliyosema dhidi ya milima ya Israeli. Ulisema, “Wamefanyika ukiwa na kutiwa mikononi mwetu tuwararue.” [13] Ulijigamba dhidi yangu na kusema maneno dhidi yangu bila kujizuia, nami nikayasikia. [14] Hili ndilo BWANA Mwenyezi asemalo: Wakati dunia yote inashangilia nitakufanya ukiwa. [15] Kwa sababu ulishangilia wakati urithi wa nyumba ya Israeli ulipofanyika ukiwa, hivyo ndivyo nitakavyokutendea. Utakuwa ukiwa, ee mlima Seiri, wewe na Edomu yote. Kisha ndipo watajua kuwa Mimi ndimi BWANA.’ ”

About this translation

Life Bible app icon
Get the Life Bible app Read offline, sync highlights and notes, and study with your library on any device.