Amosi 9:1-15 ONEN
[1] Nilimwona Bwana akiwa amesimama kando ya madhabahu, naye akasema: “Piga vichwa vya nguzo ili vizingiti vitikisike. Viangushe juu ya vichwa vya watu wote; na wale watakaosalia nitawaua kwa upanga. Hakuna awaye yote atakayekimbia, hakuna atakayetoroka. [2] Wajapojichimbia chini mpaka kwenye vina vya kuzimu, kutoka huko mkono wangu utawatoa. Wajapopanda juu hadi kwenye mbingu, kutoka huko nitawashusha. [3] Wajapojificha juu ya kilele cha Karmeli, huko nitawawinda na kuwakamata. Wajapojificha kutoka kwenye uso wangu katika vilindi vya bahari, huko nako nitaamuru joka kuwauma. [4] Wajapopelekwa uhamishoni na adui zao, huko nako nitaamuru upanga uwaue. Nitawakazia macho yangu kwa mabaya wala si kwa mazuri.” [5] Bwana, BWANA Mwenye Nguvu Zote, yeye agusaye dunia nayo ikayeyuka, na wote wakaao ndani mwake wakaomboleza: nayo nchi yote huinuka kama Naili, kisha hushuka kama mto wa Misri; [6] yeye ambaye hujenga jumba lake la kifalme katika mbingu na kuisimika misingi yake juu ya dunia, yeye aitaye maji ya bahari na kuyamwaga juu ya uso wa nchi: BWANA ndilo jina lake. [7] “Je, Waisraeli, ninyi si sawa kwangu kama Wakushi?” asema BWANA. “Je, sikuleta Israeli kutoka Misri, Wafilisti kutoka Kaftori, na Washamu kutoka Kiri? [8] “Hakika macho ya BWANA Mwenyezi yako juu ya ufalme wenye dhambi. Nami nitauangamiza kutoka kwenye uso wa dunia: hata hivyo sitaiangamiza kabisa nyumba ya Yakobo,” asema BWANA. [9] “Kwa kuwa nitatoa amri, na nitaipepeta nyumba ya Israeli miongoni mwa mataifa yote, kama vile nafaka ipepetwavyo katika ungo, na hakuna hata punje moja itakayoanguka chini. [10] Watenda dhambi wote miongoni mwa watu wangu watauawa kwa upanga, wale wote wasemao, ‘Maafa hayatatupata wala kutukuta.’ [11] “Katika siku ile nitaisimamisha hema ya Daudi iliyoanguka. Nitakarabati mahali palipobomoka na kujenga upya magofu yake, na kuijenga kama ilivyokuwa awali, [12] ili wapate kuyamiliki mabaki ya Edomu, na mataifa yote yale yanayobeba Jina langu,” asema BWANA ambaye atafanya mambo haya. [13] “Siku zinakuja,” asema BWANA, “wakati mvunaji atatanguliwa na mkulima, naye mpanzi atatanguliwa na yeye akamuaye zabibu. Divai mpya itadondoka kutoka milimani, na kutiririka kutoka vilima vyote. [14] Nitawarejesha tena watu wangu Israeli waliohamishwa; wataijenga tena miji iliyoachwa magofu, nao wataishi ndani mwake. Watapanda mizabibu na kunywa divai yake; watalima bustani na kula matunda yake. [15] Nitaipanda Israeli katika nchi yao wenyewe, hawatangʼolewa tena kutoka nchi ambayo nimewapa,” asema BWANA Mungu wenu.
