Amosi 5:1-27 ONEN
[1] Sikia neno hili, ee nyumba ya Israeli, ombolezo hili ninalifanya kuwahusu ninyi: [2] “Bikira Israeli ameanguka, kamwe hatainuka tena, ameachwa pweke katika nchi yake, hakuna yeyote wa kumwinua.” [3] Hili ndilo BWANA Mwenyezi asemalo: “Wakati mmoja wa miji yako utakapopeleka watu elfu moja vitani kwa ajili ya Israeli, mia moja tu watarudi; wakati mji utakapopeleka mia moja, kumi tu ndio watarudi hai.” [4] Hili ndilo BWANA asemalo kwa nyumba ya Israeli: “Nitafuteni mpate kuishi; [5] msitafute Betheli, msiende Gilgali, msisafiri kwenda Beer-Sheba. Kwa maana kwa hakika Gilgali itakwenda uhamishoni, na Betheli itafanywa kuwa si kitu.” [6] Mtafuteni BWANA mpate kuishi, au atafagia nyumba ya Yosefu kama moto; utawateketeza, nayo Betheli haitakuwa na yeyote wa kuuzima. [7] Ninyi ambao mnageuza haki kuwa uchungu na kuiangusha haki chini [8] (yeye ambaye alifanya Kilimia na Orioni, ambaye hugeuza giza kuwa mapambazuko na mchana kuwa usiku, ambaye huyaita maji ya bahari na kuyamwaga juu ya uso wa nchi: BWANA ndilo jina lake; [9] yeye hufanya maangamizo kwenye ngome na kufanya mji uliozungushiwa ngome kuwa ukiwa), [10] mnamchukia yule akemeaye mahakamani, na kumdharau yule ambaye husema kweli. [11] Mnamgandamiza maskini na kumlazimisha awape nafaka. Kwa hiyo, ingawa mmejenga majumba ya mawe ya fahari, hamtaishi ndani yake; ingawa mmepanda mashamba mazuri ya mizabibu, hamtakunywa divai yake. [12] Kwa kuwa ninajua hesabu ya makosa yenu na ukubwa wa dhambi zenu. Mmewaonea wenye haki na kupokea rushwa na kuzuia haki ya maskini mahakamani. [13] Kwa hiyo mtu mwenye busara hunyamaza kimya nyakati kama hizo, kwa kuwa nyakati ni mbaya. [14] Tafuteni mema, wala si mabaya, ili mpate kuishi. Ndipo BWANA Mungu Mwenye Nguvu Zote atakuwa pamoja nanyi, kama msemavyo yupo nanyi. [15] Yachukieni maovu, yapendeni mema; dumisheni haki mahakamani. Yamkini BWANA Mungu Mwenye Nguvu Zote atawahurumia mabaki ya Yosefu. [16] Kwa hiyo hili ndilo Bwana, BWANA Mungu Mwenye Nguvu Zote, asemalo: “Kutakuwepo maombolezo katika barabara zote na vilio vya uchungu katika njia kuu zote. Wakulima wataitwa kuja kulia, na waombolezaji waje kuomboleza. [17] Kutakuwepo kuomboleza katika mashamba yote ya mizabibu, kwa kuwa nitapita katikati yenu,” asema BWANA. [18] Ole wenu ninyi mnaoitamani siku ya BWANA! Kwa nini mnaitamani siku ya BWANA? Siku hiyo itakuwa giza, si nuru. [19] Itakuwa kama vile mtu aliyemkimbia simba kumbe akakutana na dubu, kama vile mtu aliyeingia nyumbani mwake na kuupumzisha mkono wake kwenye ukuta, kumbe akaumwa na nyoka. [20] Je, siku ya BWANA haitakuwa giza, na si nuru: giza nene, bila mwonzi wa mwanga? [21] “Ninachukia, ninazidharau sikukuu zenu za dini; siwezi kuvumilia makusanyiko yenu. [22] Hata ingawa mnaniletea sadaka zenu za kuteketezwa na sadaka za nafaka, sitazikubali. Ingawa mnaniletea sadaka nzuri za amani, sitazitambua. [23] Niondoleeni kelele za nyimbo zenu! Sitasikiliza sauti za vinubi vyenu. [24] Lakini acheni haki itiririke kama mto, na uadilifu uwe kama kijito kisichokauka! [25] “Je, mliniletea dhabihu na sadaka kwa miaka arobaini kule jangwani, ee nyumba ya Israeli? [26] Mmeyainua madhabahu ya mfalme wenu, Sikuthi mungu wenu mtawala, na Kiuni mungu wenu wa nyota, ambao mliwatengeneza wenyewe. [27] Kwa sababu hiyo nitawapeleka uhamishoni mbali kupita Dameski,” asema BWANA, ambaye jina lake ni Mungu Mwenye Nguvu Zote.
