[1] Kama watendakazi pamoja na Mungu, tunawasihi msipokee neema ya Mungu bure. [2] Kwa maana asema: “Wakati wangu uliokubalika nilikusikia, siku ya wokovu nilikusaidia.” Tazama, wakati uliokubalika ndio huu, siku ya wokovu ndiyo sasa. [3] Hatuweki kitu cha kukwaza katika njia ya mtu yeyote, ili huduma yetu isionekane kuwa na lawama. [4] Bali kama watumishi wa Mungu tuonyeshe kwa kila njia: katika saburi nyingi; katika dhiki, katika misiba, na katika shida; [5] katika kupigwa, katika kufungwa gerezani na katika ghasia; katika kazi ngumu, katika kukesha na katika kufunga; [6] katika utakatifu, katika ufahamu, katika uvumilivu, na katika utu wema; katika Roho Mtakatifu na upendo wa kweli; [7] katika maneno ya kweli na katika nguvu za Mungu, kwa silaha za haki za mkono wa kuume na za mkono wa kushoto; [8] katika utukufu na katika kudharauliwa; katika sifa mbaya na katika sifa nzuri; tukiwa kama wadanganyaji, lakini tukiwa wakweli; [9] tukiwa maarufu, lakini tukihesabiwa kama tusiojulikana; tukiwa kama wanaokufa, lakini tunaishi; tukipigwa, lakini hatuuawi; [10] tukiwa kama wenye huzuni, lakini siku zote tukifurahi; tukionekana maskini, lakini tukitajirisha wengi; tukiwa kama wasio na kitu, lakini tuna vitu vyote. [11] Tumesema nanyi wazi, enyi Wakorintho na kuwafungulieni mioyo yetu wazi kabisa. [12] Sisi hatujizuii kuwapenda, bali ninyi mmeuzuia upendo wenu kwetu. [13] Sasa nasema, kama na watoto wangu: Ninyi pia ifungueni mioyo yenu kabisa. [14] Msifungiwe nira pamoja na watu wasioamini, kwa jinsi isivyo sawasawa, kwa maana pana uhusiano gani kati ya haki na uovu? Au kuna ushirika gani kati ya nuru na giza? [15] Kuna mapatano gani kati ya Kristo na Beliari? Yeye aaminiye ana sehemu gani na yeye asiyeamini? [16] Kuna mapatano gani kati ya Hekalu la Mungu na sanamu? Kwa kuwa sisi tu Hekalu la Mungu aliye hai. Kama Mungu alivyosema: “Nitakaa pamoja nao na kutembea katikati yao, nami nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu.” [17] “Kwa hiyo tokeni miongoni mwao, mkatengwe nao, asema Bwana. Msiguse kitu chochote kilicho najisi, nami nitawakaribisha.” [18] “Mimi nitakuwa Baba kwenu, nanyi mtakuwa wanangu na binti zangu, asema Bwana Mwenyezi.”