2 Samweli 5:1-25 ONEN
[1] Makabila yote ya Israeli yakamjia Daudi huko Hebroni na kumwambia, “Sisi tu nyama yako na damu yako hasa. [2] Zamani, wakati Sauli alikuwa mfalme juu yetu, wewe ndiwe uliyeiongoza Israeli vitani. Naye BWANA alikuambia, ‘Wewe utawachunga watu wangu Israeli, na utakuwa mtawala wao.’ ” [3] Wazee wote wa Israeli wakamwendea Mfalme Daudi huko Hebroni, mfalme akafanya mapatano nao huko Hebroni mbele za BWANA, nao wakamtia Daudi mafuta kuwa mfalme wa Israeli. [4] Daudi alikuwa na miaka thelathini alipoanza kutawala, naye akatawala Israeli miaka arobaini. [5] Huko Hebroni alitawala Yuda kwa miaka saba na miezi sita, na katika Yerusalemu alitawala Israeli yote na Yuda kwa miaka thelathini na mitatu. [6] Mfalme na watu wake wakaenda Yerusalemu kuwashambulia Wayebusi walioishi humo. Wayebusi wakamwambia Daudi, “Wewe hutaingia humu, kwani hata vipofu na viwete wanaweza kukufukuza.” Walidhani, “Daudi hawezi kuingia humu.” [7] Hata hivyo, Daudi akaiteka ngome ya Sayuni, Mji wa Daudi. [8] Siku ile, Daudi akasema, “Yeyote ambaye atawashinda Wayebusi, atatumia huo mfereji kuwafikia hao ‘viwete na vipofu’ ambao ni adui za Daudi.” Ndiyo sababu wanasema, “ ‘Vipofu na viwete’ hawataingia kwenye jumba la ufalme.” [9] Ndipo Daudi akafanya makao ndani ya ngome na kuiita Mji wa Daudi. Akajenga eneo linalozunguka kuanzia Milo kuelekea ndani. [10] Daudi akazidi kuwa na nguvu zaidi na zaidi, kwa sababu BWANA Mungu Mwenye Nguvu Zote alikuwa pamoja naye. [11] Basi Hiramu mfalme wa Tiro akawatuma wajumbe kwa Daudi, wakiwa na magogo ya mierezi, maseremala na waashi, nao wakajenga jumba la kifalme kwa ajili ya Daudi. [12] Naye Daudi akafahamu kuwa BWANA amemwimarisha kuwa mfalme juu ya Israeli na ameinua ufalme wake kwa ajili ya Israeli, watu wake. [13] Baada ya Daudi kuondoka Hebroni, akajitwalia masuria zaidi na wake huko Yerusalemu, nao wana na binti wengi walizaliwa kwake. [14] Haya ndiyo majina ya watoto waliozaliwa kwake huko: Shamua, Shobabu, Nathani, Solomoni, [15] Ibihari, Elishua, Nefegi, Yafia, [16] Elishama, Eliada na Elifeleti. [17] Wafilisti waliposikia kuwa Daudi ametiwa mafuta kuwa mfalme wa Israeli, wakapanda na jeshi lao lote kwenda kumsaka, lakini Daudi akapata habari hizo, naye akateremka kwenye ngome. [18] Basi Wafilisti walikuwa wamekuja na kusambaa kwenye Bonde la Warefai, [19] kwa hiyo Daudi akamuuliza BWANA, “Je, niende kuwashambulia Wafilisti? Je, utawatia mikononi mwangu?” BWANA akamjibu, “Nenda, kwa maana hakika nitawatia Wafilisti mikononi mwako.” [20] Ndipo Daudi akaenda mpaka Baal-Perasimu, na huko akawashinda Wafilisti. Akasema, “Kama mafuriko yafurikavyo, BWANA amewafurikia adui zangu mbele yangu.” Kwa hiyo mahali hapo pakaitwa Baal-Perasimu. [21] Wafilisti wakaiacha miungu yao huko, naye Daudi na watu wake wakaichukua. [22] Wafilisti walikwea kwa mara nyingine na kusambaa katika Bonde la Warefai. [23] Kwa hiyo Daudi akamuuliza BWANA, naye akamjibu, “Usipande moja kwa moja, bali wazungukie kwa nyuma na uwashambulie mbele ya miti ya miforosadi. [24] Mara utakaposikia sauti ya kutembea kutoka kwenye vilele vya miti ya miforosadi, nenda haraka, kwa sababu hiyo itamaanisha kuwa BWANA ametangulia mbele yako kupiga jeshi la Wafilisti.” [25] Basi Daudi akafanya kama BWANA alivyomwagiza, naye akawaangusha Wafilisti njia yote kuanzia Geba hadi Gezeri.
