2 Samweli 22:1-51 ONEN
[1] Daudi alimwimbia BWANA maneno ya wimbo huu wakati BWANA alipomwokoa mikononi mwa adui zake wote, na pia mkononi mwa Sauli. [2] Akasema: “BWANA ni mwamba wangu, ngome yangu na mwokozi wangu, [3] Mungu wangu ni mwamba wangu, ambaye kwake ninakimbilia, ngao yangu na pembe ya wokovu wangu. Yeye ni ngome yangu, kimbilio langu na mwokozi wangu, huniokoa kutoka kwa watu wenye jeuri. [4] Ninamwita BWANA, anayestahili kusifiwa, nami ninaokolewa kutoka kwa adui zangu. [5] “Mawimbi ya mauti yalinizunguka, mafuriko ya maangamizi yalinilemea. [6] Kamba za kuzimu zilinizunguka, mitego ya mauti ilinikabili. [7] Katika shida yangu nalimwita BWANA, nilimlilia Mungu wangu. Kutoka Hekaluni mwake alisikia sauti yangu, kilio changu kikafika masikioni mwake. [8] “Dunia ilitetemeka na kutikisika, misingi ya mbingu ikatikisika, vilitetemeka kwa sababu alikuwa amekasirika. [9] Moshi ukapanda kutoka puani mwake, moto uteketezao ukatoka kinywani mwake, makaa ya moto yawakayo yakatoka ndani mwake. [10] Akazipasua mbingu akashuka chini, mawingu meusi yalikuwa chini ya miguu yake. [11] Alipanda juu ya kerubi akaruka, akapaa juu kwa mbawa za upepo. [12] Alifanya giza hema lake la kujifunika: mawingu meusi ya mvua ya angani. [13] Kutokana na mwanga wa uwepo wake mawingu yalisogea, ikanyesha mvua ya mawe na umeme wa radi. [14] BWANA alinguruma kutoka mbinguni, sauti ya Aliye Juu Sana ilisikika. [15] Aliipiga mishale na kutawanya adui, umeme wa radi na kuwafukuza. [16] Mabonde ya bahari yalifunuliwa, na misingi ya dunia ikawa wazi kwa kukaripia kwake BWANA, kwa uvumi wa pumzi kutoka puani mwake. [17] “Alinyoosha mkono kutoka juu na kunishika; alinitoa kutoka kilindi cha maji makuu. [18] Aliniokoa kutoka adui wangu mwenye nguvu nyingi, kutoka adui zangu waliokuwa na nguvu nyingi kuliko mimi. [19] Walinikabili siku ya msiba wangu, lakini BWANA alikuwa msaada wangu. [20] Alinileta nje mahali penye nafasi tele, akaniokoa kwa kuwa alipendezwa nami. [21] “BWANA alinitendea sawasawa na uadilifu wangu; sawasawa na usafi wa mikono yangu amenilipa. [22] Kwa maana nimezishika njia za BWANA; sijatenda ubaya nikamwacha Mungu wangu. [23] Sheria zake zote zi mbele yangu, wala sijayaacha maagizo yake. [24] Nimekuwa sina hatia mbele zake, nami nimejilinda nisitende dhambi. [25] BWANA amenilipa sawasawa na uadilifu wangu, sawasawa na usafi wangu machoni pake. [26] “Kwa yeye aliye mwaminifu unajionyesha kuwa mwaminifu, kwa asiye na hatia unajionyesha kutokuwa na hatia, [27] kwa aliye mtakatifu unajionyesha kuwa mtakatifu, lakini kwa aliyepotoka unajionyesha kuwa mkaidi. [28] Wewe huwaokoa wanyenyekevu, lakini macho yako ni juu ya wenye kiburi ili uwashushe. [29] Wewe ni taa yangu, Ee BWANA. BWANA hulifanya giza langu kuwa mwanga. [30] Kwa msaada wako naweza kushinda jeshi, nikiwa pamoja na Mungu wangu nitaweza kuruka ukuta. [31] “Kuhusu Mungu, njia yake ni kamilifu; neno la BWANA halina dosari. Yeye ni ngao kwa wote wanaokimbilia kwake. [32] Kwa maana ni nani aliye Mungu zaidi ya BWANA? Ni nani aliye Mwamba isipokuwa Mungu wetu? [33] Mungu ndiye anivikaye nguvu na kufanya njia yangu kuwa kamilifu. [34] Huifanya miguu yangu kama miguu ya kulungu, huniwezesha kusimama mahali palipo juu. [35] Huifundisha mikono yangu kupigana vita; mikono yangu inaweza kupinda upinde wa shaba. [36] Hunipa ngao yako ya ushindi, unajishusha chini ili kuniinua. [37] Huyapanua mapito yangu, ili miguu yangu isiteleze. [38] “Niliwafuatia adui zangu na nikawaseta, sikurudi nyuma mpaka walipoangamizwa. [39] Niliwaseta kabisa, nao hawakuweza kuinuka tena; walianguka chini ya miguu yangu. [40] Ulinivika nguvu kwa ajili ya kupigana vita; uliwafanya adui zangu wasujudu miguuni pangu. [41] Uliwafanya adui zangu wageuke na kukimbia, nami nikawaangamiza adui zangu. [42] Walipiga yowe, lakini hapakuwepo na yeyote wa kuwaokoa; walimlilia BWANA, lakini hakuwajibu. [43] Niliwaponda kama mavumbi ya nchi; niliwaponda na kuwakanyaga kama tope barabarani. [44] “Umeniokoa kutokana na mashambulizi ya watu wangu; umenihifadhi mimi kama kiongozi wa mataifa. Watu ambao sikuwajua wananitumikia, [45] nao wageni huja wakininyenyekea, mara wanisikiapo, hunitii. [46] Wote wanalegea, wanatoka katika ngome zao wakitetemeka. [47] “BWANA yu hai! Sifa ni kwa Mwamba wangu! Atukuzwe Mungu, Mwamba, Mwokozi wangu! [48] Yeye ndiye Mungu anilipiziaye kisasi, ayawekaye mataifa chini yangu, [49] aniwekaye huru toka kwa adui zangu. Uliniinua juu ya adui zangu; uliniokoa toka kwa watu wajeuri. [50] Kwa hiyo nitakusifu, Ee BWANA, katikati ya mataifa; nitaliimbia sifa jina lako. [51] Humpa mfalme wake ushindi mkuu; huonyesha fadhili zake kwa mpakwa mafuta wake, kwa Daudi na wazao wake milele.”
