[1] Yehoshafati mwanawe akawa mfalme baada yake na akajiimarisha dhidi ya Israeli. [2] Akaweka jeshi katika miji yote ya Yuda yenye ngome na kuweka askari walinzi katika Yuda na katika miji ya Efraimu ile ambayo baba yake Asa alikuwa ameiteka. [3] BWANA Mungu alikuwa na Yehoshafati kwa sababu katika miaka yake ya mwanzoni alienenda katika njia za Daudi baba yake. Hakutafuta Mabaali [4] bali alimtafuta Mungu wa baba yake na kuzifuata amri zake badala ya kufuata desturi za watu wa Israeli. [5] Kwa hiyo BWANA akauimarisha ufalme chini ya uongozi wake, nao Yuda wote wakamletea Yehoshafati zawadi, hivyo akawa na utajiri mwingi na heshima. [6] Moyo wake ukawa hodari katika njia za BWANA na zaidi ya yote, akaondoa mahali pa juu pa kuabudia miungu na nguzo za Maashera katika Yuda. [7] Katika mwaka wa tatu wa utawala wa akatuma maafisa wake ambao ni: Ben-Haili, Obadia, Zekaria, Nethaneli na Mikaya ili kufundisha katika miji ya Yuda. [8] Pamoja nao walikuwepo Walawi fulani nao ni: Shemaya, Nethania, Zebadia, Asaheli, Shemiramothi, Yehonathani, Adoniya, Tobia, Tob-Adonia, pamoja nao walikuwepo makuhani Elishama na Yehoramu. [9] Wakafundisha Yuda yote, wakiwa wamechukua Kitabu cha Sheria ya BWANA wakazunguka miji yote ya Yuda na kufundisha watu. [10] Hofu ya BWANA ikawa juu ya falme zote za nchi zilizozunguka Yuda, hivyo hawakufanya vita na Yehoshafati. [11] Baadhi ya Wafilisti wakamletea Yehoshafati zawadi na fedha kama ushuru, nao Waarabu wakamletea mifugo: kondoo dume 7,700 na mbuzi 7,700. [12] Yehoshafati akaendelea kupata nguvu zaidi na zaidi, akajenga ngome na miji ya hazina katika Yuda [13] na akawa na wingi mkubwa wa vitu katika miji ya Yuda. Pia aliweka askari wa vita wenye uzoefu huko Yerusalemu. [14] Wakaandikishwa katika jamaa zao kama ifuatavyo: Kutoka Yuda, majemadari wa vikosi vya elfu: Jemadari Adna akiwa na askari wa vita 300,000; [15] aliyefuata ni jemadari Yehohanani, akiwa na askari 280,000 walio tayari kwa vita; [16] aliyefuata ni Amasia mwana wa Zikri, ambaye alijitolea kwa ajili ya kazi ya BWANA, akiwa na askari 200,000. [17] Kutoka Benyamini: Eliada, askari shujaa akiwa na watu 200,000 wenye silaha za nyuta na ngao; [18] aliyefuata ni Yehozabadi, akiwa na askari 180,000 wenye silaha za vita. [19] Hawa ndio waliomtumikia mfalme, mbali na wale mfalme aliweka katika miji yenye ngome huko Yuda yote.