[1] Basi, ndugu, kwa habari ya nyakati na majira hatuna haja ya kuwaandikia, [2] kwa kuwa mnajua vyema kwamba siku ya Bwana itakuja kama mwizi ajapo usiku. [3] Wakati watu wanaposema, “Kuna amani na salama,” maangamizi huwajia ghafula, kama vile utungu umjiavyo mwanamke mwenye mimba; nao hakika hawatatoroka. [4] Bali ninyi, ndugu, hampo gizani hata siku ile iwakute ghafula kama mwizi. [5] Ninyi nyote ni wana wa nuru na wana wa mchana. Sisi si wana wa giza wala wa usiku. [6] Kwa hiyo basi, tusilale kama watu wengine walalavyo, bali tukeshe na kuwa na kiasi. [7] Kwa kuwa wote walalao hulala usiku na wale walewao hulewa usiku. [8] Lakini kwa kuwa sisi ni wana wa mchana, basi tuwe na kiasi, tukijivika imani na upendo kama dirii kifuani na tumaini letu la wokovu kama chapeo. [9] Kwa maana Mungu hakutuita ili tupate ghadhabu bali tupate wokovu kwa njia ya Bwana wetu Yesu Kristo. [10] Yeye alikufa kwa ajili yetu ili hata kama tuko macho au tumelala, tupate kuishi pamoja naye. [11] Kwa hiyo farijianeni na kujengana, kama vile mnavyofanya sasa. [12] Sasa tunawaomba, ndugu, waheshimuni wale wanaofanya kazi kwa bidii miongoni mwenu, wale ambao wana mamlaka juu yenu katika Bwana na ambao wanawaonya. [13] Waheshimuni sana katika upendo kwa ajili ya kazi zao. Ishini kwa amani ninyi kwa ninyi. [14] Nasi twawasihi, ndugu, waonyeni walio wavivu, watieni moyo waoga, wasaidieni wanyonge na kuwavumilia watu wote. [15] Angalieni kuwa mtu asimlipe mwenzake maovu kwa maovu, bali siku zote tafuteni kutendeana mema ninyi kwa ninyi na kwa watu wote. [16] Furahini siku zote; [17] ombeni bila kukoma; [18] shukuruni kwa kila jambo, kwa maana haya ndiyo mapenzi ya Mungu kwa ajili yenu katika Kristo Yesu. [19] Msiuzime moto wa Roho Mtakatifu; [20] msiyadharau maneno ya unabii. [21] Jaribuni kila kitu. Yashikeni yaliyo mema. [22] Jiepusheni na uovu wa kila namna. [23] Mungu mwenyewe, Mungu wa amani, awatakase ninyi kabisa. Nanyi mhifadhiwe roho zenu, nafsi zenu na miili yenu, bila kuwa na lawama katika Bwana wetu Yesu Kristo. [24] Yeye aliyewaita ni mwaminifu naye atafanya hayo. [25] Ndugu, tuombeeni. [26] Wasalimuni ndugu wote kwa busu takatifu. [27] Nawaagizeni mbele za Bwana mhakikishe kuwa ndugu wote wanasomewa barua hii. [28] Neema ya Bwana wetu Yesu Kristo iwe nanyi. Amen.