[1] Awali ya yote, nasihi kwamba dua, sala, maombezi na shukrani zifanyike kwa ajili ya watu wote: [2] kwa ajili ya wafalme na wale wote wenye mamlaka, ili tupate kuishi kwa amani na utulivu, katika uchaji wote wa Mungu na utakatifu. [3] Jambo hili ni jema, tena linapendeza machoni pa Mungu Mwokozi wetu, [4] anayetaka watu wote waokolewe na wafikie kuijua kweli. [5] Kwa maana kuna Mungu mmoja na mpatanishi mmoja kati ya Mungu na wanadamu, yaani mwanadamu Kristo Yesu, [6] aliyejitoa mwenyewe kuwa fidia kwa ajili ya wanadamu wote: jambo hili lilishuhudiwa kwa wakati wake ufaao. [7] Nami kwa kusudi hili nimewekwa niwe mhubiri na mtume (nasema kweli katika Kristo wala sisemi uongo), mwalimu wa watu wa Mataifa katika imani na kweli. [8] Nataka kila mahali wanaume wasali wakiinua mikono mitakatifu pasipo hasira wala kugombana. [9] Vivyo hivyo nataka wanawake wajipambe kwa adabu na kwa heshima katika mavazi yanayostahili, si kwa kusuka nywele, kuvalia dhahabu, lulu au mavazi ya gharama kubwa, [10] bali kwa matendo mazuri kama iwapasavyo wanawake wanaokiri kuwa wanamcha Mungu. [11] Mwanamke na ajifunze kwa utulivu na kwa utiifu wote. [12] Simpi mwanamke ruhusa ya kufundisha au kuwa na mamlaka juu ya mwanaume. Mwanamke inampasa kukaa kimya. [13] Kwa maana Adamu aliumbwa kwanza, kisha Eva. [14] Wala si Adamu aliyedanganywa, bali ni mwanamke aliyedanganywa akawa mkosaji. [15] Lakini mwanamke ataokolewa kwa kuzaa kwake, kama wakiendelea kudumu katika imani, upendo na utakatifu, pamoja na kuwa na kiasi.