1 Samweli 3:1-21 ONEN
[1] Kijana Samweli alihudumu mbele za BWANA chini ya Eli. Katika siku zile neno la Mungu lilikuwa adimu, hapakuwepo na maono mengi. [2] Usiku mmoja Eli, ambaye macho yake yalikuwa yamefifia sana kiasi kwamba aliona kwa shida sana, alikuwa amelala mahali pake pa kawaida. [3] Taa ya Mungu bado ilikuwa haijazimika, na Samweli alikuwa amelala Hekaluni mwa BWANA, ambapo Sanduku la Mungu lilikuwako. [4] Kisha BWANA akamwita Samweli. Samweli akajibu, “Mimi hapa.” [5] Naye akakimbia kwa Eli na kumwambia, “Mimi hapa, kwa kuwa umeniita.” Lakini Eli akasema, “Sikukuita; rudi ukalale.” Hivyo akaenda kulala. [6] BWANA akaita tena, “Samweli!” Naye Samweli akaamka, kwenda kwa Eli na kusema, “Mimi hapa, kwa kuwa umeniita.” Eli akasema, “Mwanangu, sikukuita, rudi ukalale.” [7] Wakati huu Samweli alikuwa bado hajamjua BWANA. Neno la BWANA lilikuwa bado halijafunuliwa kwake. [8] BWANA akamwita Samweli mara ya tatu, naye Samweli akaamka kwenda kwa Eli na kusema, “Mimi hapa, kwa kuwa umeniita.” Ndipo Eli akatambua kuwa BWANA alikuwa akimwita kijana. [9] Hivyo Eli akamwambia Samweli, “Nenda ukalale, na kama akikuita, sema, ‘Nena BWANA, kwa kuwa mtumishi wako anasikiliza.’ ” Hivyo Samweli akaenda na kulala mahali pake. [10] BWANA akaja akasimama hapo, akiita kama mara zile nyingine, “Samweli! Samweli!” Kisha Samweli akasema, “Nena BWANA, kwa kuwa mtumishi wako anasikiliza.” [11] Naye BWANA akamwambia Samweli: “Tazama, nipo karibu kufanya kitu katika Israeli ambacho kitafanya masikio ya kila mmoja atakayesikia yawashe. [12] Wakati huo nitatimiza dhidi ya Eli kila kitu nilichonena dhidi ya jamaa yake, kuanzia mwanzo mpaka mwisho. [13] Kwa kuwa nilimwambia kwamba ningehukumu jamaa yake milele kwa sababu ya dhambi aliyoijua, wanawe kumkufuru Mungu, naye akashindwa kuwazuia. [14] Kwa hiyo, nikaapa kuhusu nyumba ya Eli, ‘Hatia ya nyumba ya Eli kamwe haitaweza kufidiwa kwa dhabihu au sadaka.’ ” [15] Samweli akalala mpaka asubuhi, kisha akafungua milango ya nyumba ya BWANA. Aliogopa kumwambia Eli yale maono, [16] lakini Eli akamwita na kumwambia, “Samweli mwanangu.” Samweli akamjibu, “Mimi hapa.” [17] Eli akamuuliza, “Ni nini alichokuambia? Usinifiche. BWANA na ashughulike nawe, tena kwa ukali, kama utanificha chochote alichokuambia.” [18] Kwa hiyo Samweli akamwambia kila kitu, bila kumficha chochote. Ndipo Eli akasema, “Yeye ni BWANA; na afanye lile lililo jema machoni pake!” [19] BWANA alikuwa pamoja na Samweli alipokuwa akikua, na hakuacha hata moja ya maneno yake lianguke chini. [20] Nao Israeli wote kuanzia Dani hadi Beer-Sheba wakatambua kuwa Samweli amethibitishwa kuwa nabii wa BWANA. [21] BWANA akaendelea kutokea huko Shilo, na huko kujidhihirisha kwa Samweli kwa njia ya neno lake.
