1 Samweli 15:1-35 ONEN
[1] Samweli akamwambia Sauli, “Mimi ndiye ambaye BWANA alinituma nikutie mafuta uwe mfalme juu ya watu wake Israeli, basi sasa sikiliza ujumbe kutoka kwa BWANA. [2] Hili ndilo BWANA Mwenye Nguvu Zote asemalo: ‘Nitawaadhibu Waamaleki kwa kile walichowatendea Israeli walipowavizia wakati walipanda kutoka Misri. [3] Basi sasa nenda ukawashambulie Waamaleki na kuwaangamiza kabisa pamoja na kila kitu kilicho mali yao. Usiwahurumie; waue wanaume na wanawake, watoto na wanyonyao, ngʼombe na kondoo, ngamia na punda.’ ” [4] Ndipo Sauli akawaita watu na kuwapanga huko Telaimu, askari wa miguu 200,000 pamoja na watu 10,000 kutoka Yuda. [5] Sauli akaenda katika mji wa Amaleki na kuwavizia bondeni. [6] Kisha akawaambia Wakeni, “Ondokeni, waacheni Waamaleki ili nisije nikawaangamiza ninyi pamoja nao, kwa kuwa ninyi mliwatendea mema Waisraeli wote wakati walipanda kutoka Misri.” Basi Wakeni wakaondoka, wakawaacha Waamaleki. [7] Ndipo Sauli akawashambulia Waamaleki toka Havila mpaka Shuri, hadi mashariki ya Misri. [8] Akamchukua Agagi, mfalme wa Waamaleki akiwa hai, nao watu wake wote akawaangamiza kabisa kwa upanga. [9] Lakini Sauli na hilo jeshi wakamhifadhi hai Agagi na kondoo na ngʼombe walio wazuri, mafahali na wana-kondoo walionona kila kitu kilichokuwa kizuri. Hivi vitu hawakuwa radhi kuviangamiza kabisa, bali kila kitu kilichodharauliwa na kilicho dhaifu wakakiangamiza kabisa. [10] Kisha neno la BWANA likamjia Samweli kusema: [11] “Ninasikitika kwamba nimemfanya Sauli kuwa mfalme, kwa sababu ameacha kunifuata mimi na hakutimiza maagizo yangu.” Samweli akafadhaika, naye akamlilia BWANA usiku ule wote. [12] Asubuhi na mapema Samweli akaamka kwenda kukutana na Sauli, lakini akaambiwa, “Sauli amekwenda Karmeli. Huko amesimamisha mnara kwa heshima yake mwenyewe naye ameendelea na kuteremkia Gilgali.” [13] Samweli alipomfikia, Sauli akamwambia, “BWANA akubariki! Nimetimiza yale BWANA aliniagiza.” [14] Lakini Samweli akasema, “Nini basi huu mlio wa kondoo masikioni mwangu? Huu mlio wa ngʼombe ninaousikia ni kitu gani?” [15] Sauli akajibu, “Askari wamewaleta kutoka kwa Waamaleki, waliwaacha wale kondoo na ngʼombe wazuri ili kuwatoa dhabihu kwa BWANA, Mungu wako, lakini tuliwaangamiza kabisa wengine wote.” [16] Samweli akamwambia Sauli, “Ngoja! Nami nitakuambia lile BWANA aliloniambia usiku huu.” Sauli akajibu, “Niambie.” [17] Samweli akamwambia, “Ingawa zamani ulijiona mdogo machoni pako mwenyewe, Je, hukuwa kiongozi wa kabila za Israeli? BWANA alikutia mafuta kuwa mfalme juu ya Israeli. [18] Naye akakutuma kwa kazi maalum, akisema, ‘Nenda ukaangamize kabisa wale watu waovu, wale Waamaleki, upigane nao vita mpaka utakapowaangamiza kabisa.’ [19] Kwa nini hukumtii BWANA? Kwa nini ulivamia nyara na kufanya uovu machoni pa BWANA?” [20] Sauli akasema, “Lakini nilimtii BWANA. Nilikamilisha ile kazi ambayo BWANA alinituma. Niliwaangamiza Waamaleki kabisa na kumleta Agagi mfalme wao. [21] Askari walichukua kondoo na ngʼombe kutoka kwenye nyara, zile ambazo ni nzuri sana zimewekwa wakfu kwa Mungu, ili zitolewe dhabihu kwa BWANA Mungu wako huko Gilgali.” [22] Lakini Samweli akajibu: “Je, BWANA anafurahia sadaka za kuteketezwa na dhabihu kama vile kuitii sauti ya BWANA? Kutii ni bora zaidi kuliko dhabihu, nako kusikia ni bora kuliko mafuta ya kondoo dume. [23] Kwa maana kuasi ni kama dhambi ya uaguzi, nao ukaidi ni kama uovu wa kuabudu sanamu. Kwa sababu umelikataa neno la BWANA, naye amekukataa wewe kuendelea kuwa mfalme.” [24] Ndipo Sauli akamwambia Samweli, “Nimetenda dhambi. Nimevunja amri ya BWANA na maagizo yako. Niliwaogopa watu na kwa hiyo nikafanya walivyotaka. [25] Sasa ninakusihi usamehe dhambi yangu, nawe urudi pamoja nami, ili nipate kumwabudu BWANA.” [26] Lakini Samweli akamwambia, “Sitarudi pamoja nawe. Umelikataa neno la BWANA, naye BWANA amekukataa wewe, usiendelee kuwa mfalme juu ya Israeli!” [27] Samweli alipogeuka ili aondoke, Sauli akangʼangʼania pindo la joho lake, nalo likararuka. [28] Samweli akamwambia, “BWANA ameurarua ufalme wa Israeli kutoka kwako leo, naye ameutia kwa mmoja wa majirani zako, aliye bora kuliko wewe. [29] Yeye aliye Utukufu wa Israeli hasemi uongo wala hana kigeugeu; kwa kuwa yeye si mwanadamu, hata abadili nia yake.” [30] Sauli akajibu, “Nimetenda dhambi. Lakini tafadhali niheshimu mbele ya wazee wa watu wangu na mbele ya Israeli; rudi pamoja nami, ili nipate kumwabudu BWANA Mungu wako.” [31] Hivyo Samweli akarudi pamoja na Sauli, naye Sauli akamwabudu BWANA. [32] Ndipo Samweli akasema, “Niletee Agagi mfalme wa Waamaleki.” Agagi akaja kwake kwa ujasiri, akifikiri, “Hakika uchungu wa mauti umepita.” [33] Lakini Samweli akasema, “Kama upanga wako ulivyofanya wanawake kufiwa na watoto wao, ndivyo mama yako atakavyokuwa hana mtoto miongoni mwa wanawake.” Naye Samweli akamuua Agagi mbele za BWANA huko Gilgali. [34] Kisha Samweli akaenda Rama, lakini Sauli akapanda nyumbani kwake huko Gibea ya Sauli. [35] Hadi siku Samweli alipofariki hakwenda kumwona Sauli tena, ingawa Samweli alimwombolezea. Naye BWANA alihuzunika kwamba alimfanya Sauli kuwa mfalme juu ya Israeli.
