[1] Basi Hiramu mfalme wa Tiro akawatuma wajumbe kwa Daudi, wakiwa na magogo ya mierezi, waashi na maseremala ili kumjengea jumba la kifalme. [2] Naye Daudi akatambua kwamba BWANA amemwimarisha kuwa mfalme juu ya Israeli na kwamba ufalme wake umetukuzwa kwa ajili ya Israeli, watu wake. [3] Huko Yerusalemu Daudi akaoa wake wengine zaidi na akawa baba wa wana na mabinti wengi. [4] Haya ndiyo majina ya watoto waliozaliwa kwake huko: Shamua, Shobabu, Nathani, Solomoni, [5] Ibihari, Elishua, Elpeleti, [6] Noga, Nefegi, Yafia, [7] Elishama, Beeliada na Elifeleti. [8] Wafilisti waliposikia kuwa Daudi ametiwa mafuta kuwa mfalme wa Israeli yote, wakapanda na jeshi lao lote kwenda kumsaka, lakini Daudi akapata habari hizo, naye akatoka ili kwenda kukabiliana nao. [9] Basi Wafilisti walikuwa wameingia na kushambulia Bonde la Warefai, [10] Hivyo Daudi akamuuliza Mungu: “Je, niende kuwashambulia hao Wafilisti? Je, utawatia mikononi mwangu?” BWANA akamjibu, “Nenda, nitawatia mikononi mwako.” [11] Hivyo Daudi pamoja na watu wake wakakwea mpaka Baal-Perasimu, akawashinda huko. Akasema, “Kama maji yafurikavyo, Mungu amewafurikia adui zangu kwa kutumia mkono wangu.” Kwa hiyo mahali pale pakaitwa Baal-Perasimu. [12] Wafilisti walikuwa wameacha miungu yao huko, Daudi akaamuru iteketezwe kwa moto. [13] Kwa mara nyingine Wafilisti wakavamia lile bonde; [14] hivyo Daudi akamuuliza Mungu tena, naye Mungu akamjibu, “Usiwapandie moja kwa moja, bali wazungukie na uwashambulie kutoka mbele ya hiyo miti ya miforosadi. [15] Mara usikiapo sauti ya kwenda juu ya hiyo miti ya miforosadi, hapo ndipo utoke upigane vita, kwa sababu hiyo itaonyesha kwamba Mungu amekutangulia ili kupiga jeshi la Wafilisti.” [16] Kwa hiyo Daudi akafanya kama alivyoagizwa na Mungu, wakalipiga jeshi la Wafilisti kuanzia Gibeoni hadi Gezeri. [17] Hivyo umaarufu wa Daudi ukaenea katika kila nchi, naye BWANA akayafanya mataifa yote kumwogopa Daudi.